Tanzania kuwa mwenyeji Mkutano wa kuchakata Data za Hali ya Hewa Duniani


Na Mwandishi wetu,

TANZANIA imekuwa mwenyeji wa mkutano wa Kamati ya Kuchakata Data za Hali ya Hewa Duniani, lengo ikiwa ni kuhakikisha data za hali ya hewa zinatumika ipasavyo na taasisi za hali ya hewa katika nchi wanachama wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) na kwa manufaa ya sekta mbalimbali. Mkutano huo unaojumuisha wajumbe kutoka nchi 12.

Akizungumzia umuhimu wa mkutano huo kwa nchinya Tanzania , Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo na Mkurugenzi wa Huduma za Utabiri kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dkt. Hamza Kabelwa, amesema kutokana na changamoto kubwa za mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi, upatikanaji data sahihi za hali ya hewa ni muhmu kwa nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania.

Amesema upatikanaji wa data sahihi unasaidia kwa kiasi kikubwa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ikatika kutoa taarifa sahihi za hali ya hewa kwa maendeleo endelevu.

“Kupitia Mkutano huu tutatangaza utalii wa nchi yetu ambapo wageni hawa watakuwa mabalozi wa vivutio vya Tanzania katika nchi zao,” amesema.

Naye, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Dkt. David Richardson, amesema Kamati anayoisimamia itajikita katika kusaidia kujenga uwezo na kusambaza taarifa za hali ya hewa kwa watumiaji wote ili kulinda maisha ya watu na mali zao.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Miundombinu WMO,Dkt. Anthony Rea amesema, majukumu ya kamati hiyo yanaenda sambamba na jitihada mbalimbali zinazoendelea kutekelezwa na WMO za kusaidia nchi katika kufanikisha upatikanaji wa data za uangazi za hali ya hewa ambazo zinazaa taarifa za hali ya hewa kwa matumizi ya nchi wanachama wa WMO.

Nchi zinazoshiriki mkutano huo unaofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Arusha (AICC) kuanzia Machi 20 hadi 24,2023 ni pamoja na Australia, Brazil, Canada, Finland, Ufaransa, Ujerumani, Korea ya Kusini, Japan, Afrika Kusini, Hispania, Uingereza na Marekani.
Previous Post Next Post