NBAA YAADHIMISHA MIAKA 50 KWA KUFANYA MATEMBEZI YA HISANI


Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mhe. Jamal Kassim Ali ameipongeza Bodi ya Taifa ya Wahasibu na wakaguzi wa hesabu Tanzania (NBAA) kwa maadhimisho ya miaka 50 na kufanya matembezi ya hisani yenye lengo kuu la kutafuta fedha ili kununua vitabu vya uhasibu kwa shule za umma.


Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa kufunga Maadhimisho hayo Novemba 12 Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mhe Jamal Kassim Ali amesema kuwa bodi mwaka huu imekuja kivingine kuonesha hatua kubwa ambayo imefikiwa ikiwemo kukuza taaluma hii ya uhasibu kwa jamii na mchango wao mkubwa wa hesabu ambayo ni nyenzo muhimu katika ukuaji wa uchumi.


"Kweli jambo la kujivunia kwenye miaka hii 50 tumepiga hatua kubwa na tunavielezo vinavyoonekana wazi na kazi kubwa vitabu hivi tulivyovipata kutoka kwa wadau na vinaekwenda kwa shule za serikali ili kujenga msingi mzuri kwa wahasibu ambao ni taifa la kesho ambao tunaanza kuwakuza kuanzia chini kabisa" amesema Jamal

Aidha, Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na wakaguzi wa hesabu (NBAA) Sylvia Temu amesema leo tumefanya matembezi ya zaidi ya kilomita 5 yenye lengo la kutafuta fedha kwa ajili ya kununua vitabu kwa shule mbalimbali za serikali ambazo kwa utafiti zinaupungufu wa vitabu vya kihada, hesabu na uhasibu.


"Leo tumetoa vitabu vitabu kwa shule tatu lakini vitabu tulivyonavyo ni zaidi ya elfu tano na tutaendelea kutoa katika shule nyingine, hivyo tunatoa ushauri wa bure kabisa juu ya uhasibu namna ya kutunza vitabu vya hesabu za fedha, masuala ya kodi na tumekuwa na makampuni zaidi ya 30 pamoja na vyuo vinavyofundisha biashara na uhasibu" amesema Temu

Kwa upande wake Ulumbi Simon kutoka Brela amesema dhumuni la kushiriki kwenye maadhimisho ya miaka 50 ya bodi ya Taifa ya wahasibu na wakaguzi wa hesabu Tanzania NBAA ni kutoa elimu na kuwaelekeza wananchi katika kusajili kampuni zao na utoaji leseni

"Hivyo tunawashauri wananchi mbalimbali kuhakikisha wanasajili makampuni yao majina yao ya biashara na huduma zao kupitia ORS ili kujihakikisha zaidi" amesema Ulumbi

Naye Kaimu Mtendaji Mkuu wa chama cha wahasibu Tanzania (TAA) Winfrida Baraguza ametoa wito kwa wahasibu na wakaguzi kuwa zikitokea nafasi kama hizi wasiache kushiriki kwa sababu ni moja ya nafasi muhimu kuigusa jamii kiujumla.
Previous Post Next Post