MAKAMU WA RAIS DKT. MPANGO AFUNGUA MAONESHO YA NANE NANE MBEYA



Na Humphrey Msechu

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.Philip Isdor Mpango leo Agosti mosi 2022 mkoani Mbeya amefungua maonesho ya Nane nane ambayo kitaifa yanafanyika katika viwanja vya John Mwakangale Jijini Mbeya.

Mhe.Dkt Mpango akiwa na Waziri wa Kilimo Mhe Hussein Bashe alikata utepe ikiwa ni ishara ya kufungua rasmi maonesho hayo kwa mwaka huu 2022.

Aidha Mhe.Dkt Mpango alitembelea mabanda mbalimbali yaliyopo katika viwanja vya maonesho likiwemo banda la Wizara ya Kilimo, banda la Mifugo na Uvuvi, TANAPA, NMB na banda la CRDB. 



Katika hotuba yake Mhe.Dkt Mpango amepongeza maandalizi mazuri yaliyofanyika na kuwapongeza wakulima, wafanyabiashara na taasisi mbalimbali kwa kushiriki katika maonesho hayo.

Aidha Mhe.Makamu wa Rais amesisitiza suala la kilimo biashara na kuwahakikisha wakulima upatikanaji wa pembejeo za kilimo na mbolea, "serikali imejipanga kuhakikisha wakulima, wafugaji wanapata pembejeo za kilimo, mbolea kwa wakati na bila usumbufu".



Kauli mbiu ya maonesho ya Nane Nane 2022 kitaifa mkoani mbeya inasema, "Ajenda 10/30: Kilimo ni Biashara, Shiriki Kuhesabiwa kwa Mipango Bora ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi na kuimarisha Usalama"
Previous Post Next Post