WANAHABARI WATAKIWA KUZIPA KIPAOMBELE TAARIFA ZA HALI YA HEWA NCHINI


Taarifa sahihi za hali ya hewa huwa na athari zake ni muhimu kupatikana kwa wakati ili kuwezesha jamii na wadau kujipanga na kuandaa shughuli za kiuchumi na kijamii katika maeneo yao.

Akizungumza leo, Mkurugenzi wa Huduma za Tabiri TMA, Dkt.Hamza Kabelwa wakati  akifungua warsha ya wanahabari kuhusu mwelekeo wa mvua za msimu kwa kipindi cha mwezi Machi hadi Mei 2022 nchini kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya hewa Tanzania.



Amewataka wanahabari kuhakikisha taarifa za hali ya hewa za kila siku ikiwa ni pamoja na taarifa za hali mbaya ya hewa zinapata nafasi katika vyombo vyao vya habari ili wananchi waweze kunufaika na taasisi hiyo katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.

Amesema TMA inamchango mkubwa katika ukuaji wa kiuchumi kwa vile huduma za hali ya hewa ni mtambuka na zinahitajika katika kila sekta.

"Mamlaka imeendelea kutoa taarifa za kila siku na tahadhari dhidi ya matukio ya hali mbaya ya hewa sambamba na kutoa huduma za hali ya hewa kwa sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii kama vile usafiri wa anga, usafiri kwenye  maji, usafiri wa nchi kavu, kilimo, mafuta na gesi, ulinzi na usalama, ujenzi, maji, nishati, utalii, maafa, viwanda , afya, mazingira, mawasiliano, bima, Taasisi za kifedha na mengineyo kwa ajili ya usalama wa watu na mali zao". Amesema



Akiwasilisha Mada yake katika warsha hiyo Mwandishi wa habari wa Mwananchi Digital Bw.Rajabu Athumani amesema Mamlaka ilitangaza na kutabiri kuweza kutokea athari ya upungufu wa malisho na maji unaoweza kutokea hasa kanda ya kaskazini ikiwemo mkoa wa Tanga,hivyo kusababisha kujitokeza kwa migogoro kati ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi.



"Limejitokeza kama Mamlaka ilivyotabiri katika Mkoa wa Tanga,kutokana na kukosekana malisho ya kutosha na maji,yalitokea mapigano ya wakulima na wafugaji katika Wilaya ya Kilindi na kusababisha kifo cha mtu mmoja wilayani humo mwezi Disemba mwaka jana,huku baadhi ya mifugo ikifa kwa kudaiwa kupewa sumu kama utabiri ulivyoeleza,kutatokea migogoro kwa watumiaji wengine wa ardhi". Amesema bw.Athumani.
Previous Post Next Post