TET YAWASILISHA RASIMU ZA MITAALA MIPYA KWA MAAFISA ELIMU WOTE NCHINI


Na Mwandishi Wetu

Taasisi ya Elimu Tanzania(TET)  leo tarehe 03/10/2023  imewasilisha Rasimu za Mitaala mipya ya Elimu kwa kwa Makatibu Tawala Wasaidizi Elimu na Maafisa Elimu wa Halmashauri zote nchini ili kuwajengea uelewa juu ya rasimu hizo katika kikao kilichofanyika jijini Dodoma.

Wasilisho hilo limefanywa na Mkurugenzi Mkuu wa  TET ,Dkt. Aneth Komba ambaye ameelezea  namna Mitaala hiyo mipya itakavyosaidia kumwandaa mwanafunzi kujitegemea na kupunguza changamoto ya ajira nchini. 


Amesema, maboresho ya Mitaala yanatekeleza agizo la  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuboresha  Elimu ili mhitimu aweze kujiajiri na  kuajiriwa baada ya kumaliza masomo.
 
Sambamba na hilo, Dkt. Komba amewaomba  Maafisa Elimu kuondoa hofu juu ya mabadiliko hayo kwani yana lengo zuri la kumuandaa  mwanafunzi kupata elimu ya kujitegemea na kuajiriwa.


Naye, Mkurugenzi wa Usimamizi wa Elimu TAMISEMI, Bw. Vicent Kayombo ameishukuru TET kwa kushiriki kikao hicho na kutoa mada hiyo muhimu kwa mustakabali wa Taifa na kuahidi kuendelea kuishirikisha TET kutoa elimu zaidi ya Mitaala mipya katika  vikao mbalimbali vya wasimamizi wa elimu hapa nchini walio chini ya TAMISEMI.
Previous Post Next Post