Na Mwandishi Wetu, Dar
Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) leo, Jumamosi, tarehe 9, Septemba 2023, kimezindua Bonanza la Waajiri (Waajiri Health Bonanza) kwa mwaka 2023 ambapo kilele chake kitafanyika tarehe 7 Oktoba 2023 katika Viwanja vya Leaders Club, Dar es Salaam ambalo litaenda sambamba na maadhimisho ya Wiki ya Huduma kwa mwaka huu 2023.
Mtendaji Mkuu wa ATE, Bi. Suzanne Ndomba-Doran amesema kuwa Bonanza la Mwaka huu limebeba kauli mbiu inayosema ”Kuimarisha Afya ya Akili ili Kuongeza Tija Mahali pa Kazi.” ikiwa na lengo la kuhamasisha umuhimu wa kuimarisha afya ya akili mahala pa kazi.
Mgeni Rasmi katika Bonanza hili atakuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa (MB)
Uzinduzi wa Bonanza hili umeenda sambamba na michezo ya mpira wa miguu ilyochezwa kati ya timu za ATE, TUCTA, OSHA, KAIRUKI na G4S Security. Kwa upande wa mpira wa pete imehusisha timu za TTCL, TPA na OSHA.