TMA YATOA UTABIRI WA MVUA ZA VULI KWA MWAKA 2023


Na Mwandishi wetu, Dar 

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesema mvua za Juu ya Wastani hadi Wastani zinatarajiwa katika maeneo mengi ya mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza, Shinyanga, kusini mwa mkoa wa Simiyu, kaskazini mwa mkoa wa Kigoma, Dar es Salaam, Tanga, Pwani (ikiwemo visiwa vya Mafia), kaskazini mwa mkoa wa Morogoro na pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba katika msimu wa mvua za Vuli, 2023. Aidha, maeneo ya mikoa ya Mara, kaskazini mwa mkoa wa Simiyu, Arusha, Manyara na Kilimanjaro yanatarajiwa kupata mvua za wastani hadi juu ya wastani.

Hayo yameelezwa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC) wakati wa mkutano na vyombo vya habari kuhusiana na mwelekeo wa msimu wa mvua za Vuli (Oktoba hadi Disemba 2023), katika ukumbi wa Ubungo Plaza,Dar es Salaam,Tarehe 24 Agosti 2023. Alifafanua kuwa kutokana na uwepo wa El-Niño, vipindi vifupi vya mvua vinatarajiwa kwa mwezi Septemba, 2023 katika baadhi ya maeneo nchini, hata hivyo, mvua za Vuli, 2023 zinatarajiwa kuanza rasmi mwezi Oktoba, 2023 katika maeneo mengi. 

“Mvua zinatarajiwa kuanza wiki ya nne ya mwezi Septemba, 2023 katika maeneo ya magharibi mwa Ziwa Victoria na kusambaa katika maeneo mengine mwezi Oktoba, 2023. Kwa kawaida mvua za Vuli huisha mwezi Disemba, hata hivyo msimu huu mvua za nje ya msimu zinatarajiwa kuendelea mwezi Januari, 2024. Ongezeko la mvua linatarajiwa mwezi Disemba, 2023”. Alisema Dkt. Chang’a.

Dkt. Chang’a alitoa wito kwa wananchi kufuatilia taarifa za utabiri wa saa24, siku 10, mwezi natahadhari zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania ikizingatiwa kuwa mwelekeo wa mvua uliotolewa ni kipindi cha msimu wa miezi mitatu, hivyo viashairia vinavyochangia mwenendo wa mifumo ya mvua na mabadaliko ya muda mfupi utazingatiwa katika uchambuzi wa utabiri wa muda wa kati na mfupi.
Previous Post Next Post