PWC yatinga hatua ya fainali ya michuano ya NBAA



Na Humphrey Msechu 

TIMU ya PWC Tanzania wameonesha ubabe katika mashindano ya maadhimisho ya miaka 50 ya NBAA kwa kuibuka na ushindi mnono wa bao 2-1 dhidi ya KPMG katika viwanja vya TPDC jijini Dar es Salaam.

Mashindano hayo yameendelea kutimua vumbi katika hatua ya nusu fainali ya kwanza kwa timu ya PWC Tanzania kutangulia fainali kwa kuwatupa nje timu ya KPMG na kwenda kushiriki nafasi ya kutafuta mshindi wa tatu.

Nahodha wa PWC Tanzania Neulis Nelson alisema walikuwa wamejiandaa vizuri zaidi ya wapinzani wao kwani hata katika hatua ya mtoano mpinzani wao alipita kwa ushindi wa mezani baada ya timu waliyotakiwa kucheza nao kutofika uwanjani.

"Mashindano yoyote lengo la kushindana ni kushinda, tumejipanga na kujiandaa kwa mchezo wa fainali ambao tutacheza siku ya jumapili" alisema Nelson

Hivyo, Nahodha Msaidizi wa timu ya KPMG Jackson Mwangingo alisema mechi ilikuwa nzuri lakini haikuwa bahati kwao kwani wapinzani wao waliweza kutumia nafasi chache na wakazitumia vyema na kuibuka na ushindi.

Aidha, Mwangingo alidai kubwa kuna tetesi huenda wapinzani wao walimchezesha mchezaji ambaye sio mfanyakazi wa timu yao, hivyo jambo hilo lichunguzwe na ikibainika kuwa ni kweli, hatua za kisheria zifuatwe na kama ni kweli wanyang'anywe ushindi na tupewe sisi.

Fainali ya Mashindano ya mpira wa miguu ya maadhimisho ya 50 ya NBAA inatarajiwa kucheza mnamo Novemba 28, 2022 majira ya saa 10 jioni katika uwanja wa TPDC jijini Dar es Salaam.
Previous Post Next Post