LIPA KWA SIMU SULUHISHO LA UPOTEVU WA PESA



Na Richard Mrusha  Arusha 

Kaimu Mkurugenzi wa Kampuni ya mawasiliano   Tigo Kanda ya Kaskazini, Daniel Mainoya, amewashauri wafanyabiashara kutumia huduma ya lipa kwa simu kwa kuwa ni salama na kujiepusha katika hatari ya kupoteza fedha.

Mainoya ameyasema hayo leo wakati akiwatembelea wateja wake waliopo katika maonesho ya Karibu Kili Fair (KKF) yaliyoanza jana katika viwanja vya Magereza Kisongo mkoani Arusha yaliyokutanisha zaidi ya kampuni 700 za kimataifa kutoka nchi zaidi ya 42.

“Huduma ya lipa kwa simu imewasaidia wafanyabiashara kwa ajili ya usalama wa fedha zao haina haja ya kubeba fedha taslimu kwa kuwa fedha zinakuwa katika simu hayupo katika hatari ya kupoteza fedha zake,”amesema.

Amesema wameshiriki katika maonesho hayo kuangalia wateja wao ambao wanatumia huduma ya lipa kwa simu ikiwemo wanauza bidhaa za asili zinazotokana na nazi.



“Tumewatembelea ili kujua changamoto ambazo wanakutana nazo ili kuwasaidia kuwahudumia wateja wetu ambao wanawatembelea katika banda lao,”amesema na kuongeza kuwa:

“Imekuwa ni kivutio kikubwa kwa wageni wanaotembelea banda hili kwa kuwa wanauza bidhaa zinazotokana na mazao ya asili sisi kama Tigo tunawawezesha ili kuwahudumia wateja kwa ubora,”.

Mainoya aliwashauri wananchi kuendelea kutembelea maonyesho hayo ambayo yamekuwa na ubora mzuri ikilinganishwa na miaka mingine.

Naye Mmiliki wa kampuni ya bidhaa za asili ya Cocozania, Mariana Soko, amesema lipa kwa Simu imesaidia usalama wa kuhifadhi fedha pindi mteja anapofanya manunuzi ya bidhaa zao.

Amesema ameishukuru kampuni ya Tigo kuwatembelea na kufuatilia changamoto ambazo zinawakabili ili kuwasaidia katika kuhakikisha wanatoa huduma bora kwa wateja wote walioshiriki maonesho hayo.

Previous Post Next Post