TPHPA yajipanga kudhibiti visumbufu vya mimea kabla ya kuleta madhara


Mwandishi Wetu, Mbeya

KAIMU Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA) Prof.Joseph Ndunguru amesema,Mamlaka hiyo kupitia wabia wake,imenunua Drons (ndege nyuki) 20 ambazo zitakuwa na kazi ya kusavei katika mashamba ya wakulima kubaini uwepo wa viashiria vya visumbufu vya mimea kudhibiti kabla ya kuleta madhara katika mimea.

Akizungumza na waandishi wa habari katika banda hilo,Prof.Ndunguru amesema,lengo la hatua hiyo ni kuleta tija kwa uwepo wa Mamlaka hiyo kwa kutumia teknolojia za kisasa kudhibiti visumbufu vya mimea kwa maana ya wadudu na magonjwa.

“Kwa hiyo hapa tunahama kutoka kwenye kusubiri tatizo litokee halafu uende lakini sasa unafanya udhibiti kabla wadudu hawajaleta madhara.”amesema Prof.Ndunguru

Kwa mujibu wa Kiongozi huyo ,pia TPHPA imenunua  vifaa mpakato kwa maana ya vipimo 19 vya kufanyia uchunguzi wa visumbufu vya mimea kwa kupima DNA zao ambavyo hutoa majibu shambani.

“Vipimo hivi vitakwambia na kukuonyesha kama ni mdudu gani, alitoka wapi ,aliingia mwaka gani na anaweza kuleta madhara gani ,na  ili kumdbiti mdudu kama huyo utumie kiuatilifu gani sahihi kinachofaa kumdhibiti,kwa hiyo hapa tutakuwa tunafanya udhibiti wa visumbufu kwa njia sahihi kabisa na siyo kubahatisha “amesisitiza

Ametumia nafasi hiyo kuwaasa wakulima na wananchi kwa ujumla kutembelea Banda hilo ili waweze elimu sahihi ya matumizi ya viuatilifu.

“Sisi tunafundisha wakulima namna ya kutumia viuatilifu kwenye mashamba yao lakini pia tunawafundisha wafanyabiashara wa viuatilifu namna ya kutambua viuatilifu bora kwa kuleta sampuli kwenye maabara zetu  ambayo imepewa ithibati kwani matokeo yanayotokana na uchambuzi kwenye maabara zetu yanakubalika tambuika dunia nzima.”

Amesema hatua hiyo inaweza kusaidia wafanyabiashara kukidhi viwango vya kimataifa vya masoko

“Kwa mfano sasa hivi Tanzania tunauza maparachichi nje ya nchi, na wanunuzi wanataka masalia ya viuatilifu yasionekane kwenye parachichi ,kwa hiyo mashine zetu ndiyo zinapima na kuhakikisha hakuna viuatilifu na hivyo kuwezesha biashara hiyo kufanyika”

Aidha Prof.Ndunguru amesema,mwanzoni watanzania walikuwa wanaenda kupima viuatilifu nje ya nchi kwa gharama kubwa lakini sasa zinapimwa hapa nchini na hivyo kuwaondolea wakulima hao adha ya kufuata huduma hiyo nje ya nchi.

Previous Post Next Post