SERIKALI IMELITAMBUA DENI LA KIWIRA COAL MINE LA SHILINGI BILIONI 1.52



Bungeni Dodoma

Naibu Waziri wa Madini Dkt.Steven Kiruswa amesema Serikali imelitambua deni la Shilingi Bilioni 1.52 lililotokana na mapunjo ya mafao kutoka kwa waliokuwa wafanyakazi na madeni ya Wazabuni wa Mgodi wa Kiwira Coal Mine kabla ya ubinafsishaji.

Dkt. Kiruswa ameyasema hayo leo Septemba 2, 2024, Bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Kyela Mhe. Ally Mlanghila Jumbe aliyetaka kujua mahali ulipofikia mchakato wa Serikali wa kuwalipa wafanyakazi hao na kuongeza kwamba, tayari deni hilo limepelekwa Hazina baada ya uhakiki kukamilika liweze kulipwa pindi fedha zitakapopatikana.

‘’Mhe. Spika, uhakiki wa madeni hayo ulibaini madai ya wafanyakazi yalikuwa shilingi bilioni 1.024 kwa wafanyakazi  893 na madeni ya wazabuni ikiwemo watoa huduma ya ulinzi yalikuwa ni shilingi milioni 496 na kufanya deni lote kuwa jumla ya shilingi bilioni 1.52,’’  amesema Dkt. Kiruswa.

Amefafanua kuwa, baada ya Chama cha Wafanyakazi Mgodini (TAMICO) kuwasilisha malalamiko ya mapunjo hayo Serikalini, Serikali ilifanya ukaguzi maalum kupitia kwa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Novemba 2008 na baadaye Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali (Internal Audit General) alihakiki madeni hayo Agosti, 2021.

Kutoka Bungeni
Previous Post Next Post