VYUO VIKUU NCHINI VYASHAURIWA KUJIIMARISHA NA KUJIENDESHA KATIKA VIWANGO VYA KIMATAIFA


Na Mwandishi Wetu

Makamu Wakuu na Marasi wa Vyuo Vikuu nchini wameshauriwa kuimarisha kusimamia na kuendesha Vyuo Vyao kwa viwango vya Kimataifa ili vionekane, vijulikane na vitambulike.

Ushauri huo umetolewa Novemba 16, 2022 Jijini Dodoma na Dkt. Francis Michael Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia wakati akizungumza na Umoja wa Makamu Wakuu na Marasi wa Vyuo Vikuu Binafsi (TAPU) ambapo amesema moja kati ya sababu za Vyuo Vikuu vya Tanzania na kwingineko barani Afrika
kutotambulika dunia ni kuendeshwa bila kujilinganisha sana na vile vyevye hadhi kubwa kimataifa na hivyo kutoonekana
kwenye ramani ya dunia. 


Ameongeza kuwa kuna namna nyingi za kufanikisha azma ya vyuo kutambulika ikiwa ni pamoja na kuweka utararibu wa kubadilishana watalaam katika maeneo yenye uhitaji na upungufu, kuwa na programu ambazo zinavutia wanafunzi wa kigeni kusoma nchini sambamba na kuwa na utaratibu wa kubadilishana wanafunzi (students exchange programs), wanataaluma wetu kuwekeza katika tafiti zenye matokeo makubwa kidunia.

" kama ambavyo Mhe. Prof. Adolf Mkenda Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia anasisitiza na kutenga fedha kwa ajili ya motisha kwa watafiti wa aina hiyo. Tafiti hizi zinatangaza sana vyuo vyetu kwa kuwa matumizi yake duniani ni makubwa" amesema Katibu Mkuu


Ameongeza kuwa ni muhimu vyuo kuingia katika mahusiano mahususi na vyuo vikuu vya nje vilivyo bora zaidi kwani kuimarika kwa mahusiano haya kuna nafasi kubwa ya kuvitangaza vyuo kimataifa na hivyo kuwa katika nafasi nzuri katika "World University Ranking". 

Aidha, Dkt Michael amesema Serikali iliridhia na kutoa leseni ya kuanzishwa Vyuo Vikuu
binafsi mwaka 1995 kwa kurekebisha Sheria ya Elimu namba10 ya mwaka 1978, na hivyo kuja na Sheria ya Elimu namba 10 ya1 995 iliyopelekea kuanzishwa kwa vyuo vikuu binafsi baada ya kutambua umuhimu wa sekta binafsi kushiriki katika utoaji wa Elimu ya Juu nchini ambapo mpaka sasa kuna vyuo vikuu 18, Vyuo Vikuu Vishiriki 10 pamoja na vituo tatu vya kufundishia (Campus and centres).


Wakati huo huo Katibu Mkuu huyo amevitaka vyuo vikuu vyote nchini kuanza kutumia programu maalumu kwa ajili ya kuangalia kiwango cha unakilishaji (plagiarism) ili kuwasaidia wanafunzi kuandika maandiko ya utafiti kwa ustadi wa hali ya juu na hivyo kuwaandaa kiushandani katika soko la ajira, lakini pia kutaka kuwepo na kiwango sawia cha uhimilivu (percentage tolerance) wa kunakilisha kusikoruhusiwa na namna bora ya matumizi ya programu hii.

Naye Mwenyekiti wa Umoja wa Makamu Wakuu na Marasi (TAPU) Pius Peter ameishukuru wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kukubali kukutana nao ili kujadili kwa pamoja changamoto mbalimbali zinazokabili Umoja huo na kuona namna bora ya kuzitatua.


Ameongeza kuwa anaishukuruu serikali kwa kukubali kuanzishwa kwa Vyuo Binafsi nchini ambavyo vinasaidia katika kutoa elimu ya juu kwa wanafinzi wapatao asilimia 32 ya wanafunzi wote wa elimu ya juu nchini.
Previous Post Next Post