Waziri wa Viwanda na Biashara, Suleimani Jafo, amezitaka taasisi zote za serikali zinazopaswa kumlinda mlaji kufanya kazi kwa pamoja kwa weledi ili kukidhi matakwa ya walaji wa bidhaa husika.
Akizungumza wakati wa Uhitumisho wa wiki ya Haki ,Mlaji kitaifa iliyofanyika jijini Dar es Salaam , Ijumaa tarehe 21 Machi, 2025, Waziri Jafo amesema kuna umuhimu wa ushirikiano kati ya mamlaka za udhibiti.
Dkt. Jafo ameziomba Shirika la Viwango Nchini (TBS), Shirika la Vipimo na Uzito (WMA), Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA), Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Mamlaka ya Mawasiliano Nchini (TCRA) na taasisi nyingine muhimu kushirikiana kuhakikisha kuwa bidhaa na huduma zinakuwa bei nafuu na za ubora wa juu zinapatikana kwa Watanzania wote.
Aidha alisisitiza kwamba Tanzania sasa ni sehemu muhimu ya Jumuiya ya Maendeleo ya Afrika Kusini (SADC), Eneo Huru la Biashara la Bara la Afrika (ACFTA), na masoko mengine ya kimataifa kwahiyo kuna umuhimu wa kumlinda mlaji katika ngazi ya kanda na kimataifa.
Awali akizungumza, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani Haki (FCC), William Erio, ameelezea umuhimu wa haki za watumiaji kimataifa, ambazo ni nguzo muhimu ya mfumo wa soko unaofanya kazi.
"Leo, tunatafakari juhudi za kimataifa zilizofanywa kulinda watumiaji, na hapa Tanzania, tunaendelea kuhakikisha kuwa mazingira ya soko letu ni ya haki, uwazi, na yanayofaa kwa biashara na watumiaji," amesema
Akizungumzia juu ya mafanikio ya FCC, amesema wamepokea cheti cha Shirika la Uthibitisho la Kimataifa (ICO), ambalo linaashiria hatua muhimu katika juhudi za tume za kupata utambuzi wa kimataifa na kujenga imani duniani.
Amesisitiza kuwa cheti cha ICO hakitasaidia tu kuboresha sifa ya soko la Tanzania, bali pia kitavutia wawekezaji wa kimataifa wanaotamani kushiriki katika soko lenye ushindani na udhibiti mzuri.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirikisho la Wenye Viwanda Nchini, Leodegar Tenga (CTI), amesema FCC imekuwa na mchango mkubwa katika kukuza ushindani mzuri katika sekta ya viwanda.
Alimpongeza FCC kwa juhudi zake za kuhamasisha bidhaa na huduma bora katika viwanda vya Tanzania.
"Ni muhimu kwa viwanda, vikubwa na vidogo, kuendelea kujitahidi kuboresha bidhaa na huduma zao ili kukidhi matarajio ya watumiaji. Jukumu la FCC katika kuhakikisha ushindani wa haki unaleta mazingira ambapo biashara zinaweza kukua huku zikilinda watumiaji," alisema Bwana Tenga.
Kwa upande wake Cynthia Bavo, Naibu Mkurugenzi wa FCS, alielezea dhamira yao ya kuwawezesha na kuwalinda walaji kwa ushirikiano na FCC na kwa ufadhili wa TradeMark Africa, itatekeleza mradi wa miaka mitatu wa ulinzi wa mlaji unaolenga kuongeza uelewa wa mlaji kuhusu haki na wajibu wao na kuimarisha mifumo ya kutatua malalamiko yao.
"Mradi unalenga kuhakikisha kwamba angalau asilimia 60 ya walaji wa Tanzania wanakuwa na taarifa za kutosha na wanalindwa kufikia mwaka 2027." Amesema Cynthia.
Sherehe ya Siku ya Haki za Watumiaji Duniani haikuwa tu ni kielelezo cha maendeleo yaliyofikiwa katika kulinda watumiaji wa Tanzania, bali pia ni wito kwa pande zote kushirikiana katika kuendeleza haki za watumiaji na usawa wa kiuchumi. Kupitia ushirikiano endelevu, elimu ya umma, na usimamizi wa sheria thabiti, Tanzania iko katika nafasi nzuri ya kujenga mazingira ya soko endelevu na rafiki kwa watumiaji kwa ajili ya siku zijazo.